Na Boazi Mazigo-Geita
Mkuu wa Mkoa Geita Mhe.Martin Shigela Agosti 23, 2022 ameshiriki kuhesabiwa pamoja na familia yake kwenye zoezi la sensa ya watu na makazi akiwa nyumbani kwake msisitizo mkuu na wito kwa wananchi ukiwa ni kutoa taarifa sahihi kwa makarani na kwamba taarifa hizo ni siri na zitaliwezesha taifa kupanga mipango ya maendeleo.
Mhe.Shigela ameeleza kufurahishwa kwake na jinsi makarani walivyoandaliwa kukusanya taarifa hizo na kwamba ni muhimu wananchi kutoa ushirikiano na taarifa sahihi kwa makarani hao.
"tunamshukuru na kumpongeza Mhe.Rais Samia kwa kuwezesha ufanikishaji zoezi hili kwa kutoa fedha na vifaa vyote vinavyohusika kwenye Sensa. Wananchi tambueni kuwa makarani wametumwa na taifa, hivyo muhimu ni kuwapa ushirikiano na taarifa sahihi ili usiwe sehemu ya kukwamisha zoezi". amesema Mhe.Shigela.
Ameongeza kuwa, taarifa zinazokusanywa zitalisaidia taifa kwa kujua akitoa mfano kuwa, katika mpango wa bima kwa kila mwanachi, serikali itajua ni kina nani wana bima na wangapi hawana lakini pia itasaidia kujua shughuli za kiuchumi walizonazo wananchi hivyo kuwa na mipango zaidi ya kuboresha maisha.
Mhe. Shigela amemaliza kwa kutoa onyo kwa wale wanaodhihaki zoezi la sensa kwa kupotosha kupitia mitandao ya kijamii hususan magrupu ya wasap akisema ni muhimu unapoona mtu ametuma taarifa za kupotosha kwenye makundi hayo basi inatakiwa kufutwa na si kuzisambaza zaidi kwani kwa kufanya hivyo ni kutenda kosa la sheria ya mtandao na hivyo kuwajibika kwayo kisha kutembelea eneo la Katoro na Chato kukagua maendeleo ya zoezi hilo.
Kwa upande mwingine, Katibu Tawala Mkoa Geita Prof.Godius Kahyarara amehesabiwa akiwa kwenye makazi yake na kuendelea kutoa wito kwa wananchi kushiriki kikamilifu kwa kutoa taarifa sahihi akitoa mfano wa taarifa muhimu za mifugo kuwezesha upatikanaji wa mifugo 30,000 inayohitajika kwenye machinjio ya kisasa Mpomvu mjini Geita
Mratibu wa Sensa Mkoa Bw.Khalid Msabaha amesema bado anaendelea kuishukuru serikali chini ya uongozi wa Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha zoezi hilo kupitia uwezeshaji wa fedha na vifaa na kwamba hakuna changamoto yoyote kukwamisha zoezi hivyo kumhakikishia mkuu wa mkoa na wananchi wa Geita kuwa wote watahesabiwa kwakuwa idadi ya makarani imewekwa kwa uwiano wa idadi ya kaya.
Aidha, Bibi Kulwa Kessy pamoja na Bw. James Shigela wakazi wa katoro kwa nyakati tofauti wamepongeza zoezi la sensa na kuendelea kutoa wito kwa wakazi wengine wote kushiriki zoezi hilo muhimu.
Akiwa wilayani Chato, Mhe.Shigela Ametembelea na kujionea zoezi hilo akipita kwenye makazi ya mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo Bw.Mandia Kihiyo ambapo akiwa katika eneo hilo, Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe.Martha Mkupasi amesema hadi muda huo, zoezi hilo limeenda vizuri na kwamba anawahakikishia wananchi wote kuwa watahesabiwa hivyo kumpongeza Mhe.Rais kwa uwezeshaji kwani hakuna changamoto yoyote iliyokwamisha zoezi.
Mbunge wa Chato Mhe.Dkt.Medard Kalemani kwa upande wake ameeleza kuwa, wananchi wameitikia kwa wingi na anamshukuru sana Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan kwaniaba ya wanachato na kwamba wamehamasika sana na kupitia hamasa waliyoifanya anaamini wote watahesabiwa.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita
Sanduku la Barua: S.L.P 315
Simu: 028 2520035
Mobile: 028 2520035
barua pepe: ras.geita@tamisemi.go.tz
Hakimiliki©2017Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita. Haki zote zimehifadhiwa