Katika kuhakikisha huduma za uchunguzi wa madini ya aina mbalimbali zinaendelea kuboreshwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan imekusudia kujenga maabara ya upimaji wa sampuli za madini katika Mkoa wa Geita.
Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde alipokuwa akizungumza na wachimbaji wadogo Wilayani Nyang’hwale kwenye kikao kilichofanyika katika mgodi wa Kasubuya kata ya Nyijundu.
Mhe. Mavunde ameeleza kuwa sekta ya Madini inategemewa sana katika kuchochea uchumi wa Nchi ya Tanzania na kwamba mchango wa wachimbaji wadogo unaotokana na shughuli za madini unaongezeka kila kukicha kutokana na maboresho makubwa ya sheria, sera yanayofanywa na Serikali ikiwemo ujenzi wa Maabara za vipimo na vifaa vya kisasa vya kupimia madini.
“Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameelekeza kufanyika kwa utafiti wa kina wa madini ambapo kwa sasa Wizara inajipanga kutekeleza mradi wa ununuzi wa helikopta kwa ajili ya kufanya utafiti wa kina wa maeneo yenye madini na kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata taarifa sahihi na kuondokana na uchimbaji wa kubahatisha.” Aliongeza Mhe. Mavunde.
Waziri wa Madini alitumia jukwaa hilo kukabidhi leseni 36 za uchimbaji wa madini kwa vikundi 10 vya wachimbaji wadogo wilayani humo na kuwaasa wamiliki wa leseni za uchimbaji madini kuzingatia sheria ya madini sura ya 123 na kanuni zake katika utekelezaji wa majukumu yao.
Mhe. Mavunde pia ametoa rai kwa wamiliki wote wenye leseni za uchimbaji kuhakikisha wanaziendeleza na sio kuzitunza ndani kwani Serikali haitarajii kuona maeneo yakishikiliwa bila kuendelezwa, akieleza kuwa ameshafuta leseni 73 zilizoshindwa kufanyiwa kazi tangu mwaka 2012 licha ya ukubwa wake kufikia ekari 741,000. Ameonya kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa wamiliki wasioendeleza maeneo.
Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale Mhe. Grace Kingalame ametoa pongezi kwa Wizara ya Madini kwa kazi kubwa wananyoifanya katika kuhakikisha sekta hiyo inawakwamua wananchi kiuchumi na kuiomba Serikali kuwapatia leseni za uchimbaji vijana na wananchi wa Nyang’hwale ili waweze kupata maeneo yatakayowawezesha kujikimu kwa sababu kwa asilimia kubwa ya uchumi wa wilaya hiyo unategemea mapato yanayotokana na sekta ya uchimbaji.
Maabara itakayojengwa katika Mkoa wa Geita ni kati ya maabara tatu zitakazojengwa katika maeneo mengine Nchini, ambapo maabara nyingine zitajengwa katika Wilaya ya Chunya na jiji la Dodoma.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita
Sanduku la Barua: S.L.P 315
Simu: 028 2520035
Mobile: 028 2520035
barua pepe: ras.geita@tamisemi.go.tz
Hakimiliki©2017Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita. Haki zote zimehifadhiwa